Nani anayeweza kuchukua nafasi ya Biden ndani ya chama cha Democratic?

ed

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Joe Biden
  • Author, Ana Faguy
  • Nafasi, BBC

Kubabaika kwa Rais wa Marekani Joe Biden wiki iliyopita katika mdahalo na Donald Tarump, kulileta mshtuko katika chama cha Democratic, na kuibua maswali kuhusu nani anaweza kuchukua nafasi yake katika tiketi ya urais iwapo ataamua kujiuzulu.

Hatua hiyo – ingawa haina dalili ya kutokea hadi sasa - inaweza kuanzisha mbio za wagombea katika chama cha Democratic, miezi michache kabla ya wapiga kura kupiga kura.

Huku Wa-democratic wakielezea hofu na wasiwasi wao juu ya mustakabali wa Biden, kuna mijadala, iwapo rais huyo mwenye umri wa miaka 81, ndiye mgombea anayefaa kukabiliana na Rais wa zamani Donald Trump mwezi Novemba.

Hawa hapa ni baadhi ya watu ambao wanaweza kuchukua nafasi yake.

Pia unaweza kusoma

Makamu wa Rais, Kamala Harris

sdc

Chanzo cha picha, Getty Images

Makamu wa Rais Kamala Harris, tayari yuko kwenye mbio za urais na Biden, ni chaguo la wazi kuchukua nafasi yake.

Akiwa makamu wa rais, amekuwa mstari wa mbele katika kampeni ya kulinda haki za uzazi baada ya Mahakama ya Juu kubatilisha haki ya kuavya mimba.

Bi Harris amethibitisha kuwa mshirika mwaminifu kwa rais na alitetea vikali uzungumzaji wake katika mdahalo. Baada ya hafla hiyo, alikiri kuwa rais alikuwa na "mwanzo wa polepole" lakini aliendelea kutoa majibu muhimu zaidi kuliko Trump.

"Watu wanaweza kujadiliana kuhusu mtindo wa uzungumzaji, lakini nani atakuwa rais wa Marekani katika uchaguzi huu, lazima hilo litokane na mambo ya maana," Harris aliiambia CNN siku ya Alhamisi.

Harris ana sifa na jina kubwa linalotokana na kazi ya makamu wa rais, lakini amekuwa na viwango vya chini vya kukubalika katika kipindi chote cha uongozi wake.

Asilimia 49 ya Wamarekani hawamuungi mkono Bi Harris, huku 39% wakimuunga mkono, kulingana na kura zilizofuatiliwa na FiveThirtyEight.

Lakini Bi Harris atakuwa na wakati mzuri kujitangaza, atakapokabiliana na mgombea mweza wa Trump, katika mdahalo utakao endeshwa na CBS, wa makamu wa ma-rais kabla ya Kongamano la Kitaifa la Democratic mwezi Agosti.

Gavana wa Michigan, Gretchen Whitmer

we

Chanzo cha picha, Getty Images

Gretchen Whitmer, gavana wa mihula miwili huko Michigan, anazidi kuwa maarufu na wadadisi wengi wanaamini atagombea urais 2028.

Amemfanyia kampeni Biden hapo awali. Aliliambia gazeti la New York Times, anataka kumuona rais wa Kizazi cha X mwaka 2028, lakini hakusema kuwa atagombea.

Mwaka 2022, aliongoza kampeni iliyokipatia chama cha Democratic, udhibiti wa bunge la jimbo la Michigan.

Udhibiti huo wa kisiasa ulimruhusu kutunga sera kadhaa, ikiwa ni pamoja na kulinda haki ya uavyaji mimba kwa watu wa Michigan na kupitisha kanuni salama za umiliki wa bunduki.

Gavana wa California, Gavin Newsom

sxc

Chanzo cha picha, Getty Images

Gavana wa California, Gavin Newsom ni mmoja wa waungaji mkono maarufu wa Utawala wa Biden. Huonekana mara kwa mara kwenye runinga akimsifu Biden.

Lakini Newsom ana malengo yake ya kisiasa.

Mara nyingi ameorodheshwa kama mgombea wa 2028, lakini wachambuzi wengi wa siasa wanaamini, anaweza kuwa bora kuchukua nafasi ya Biden sasa.

Newsom ameinua hadhi yake ya kitaifa katika miaka ya hivi karibuni kwa kuwa mzungumzaji mkuu wa chama kwenye vyombo vya habari vya kihafidhina, na kupitia mjadala dhidi ya Gavana wa Florida Ron DeSantis mwaka jana.

Waziri wa Uchukuzi, Pete Buttigieg

as

Chanzo cha picha, Getty Images

Sio siri kuwa Waziri wa Uchukuzi, Pete Buttigieg ana matarajio ya kuwa rais. Aligombea urais 2020 na mara nyingi huelezwa kama mmoja wa washirika bora wa Utawala wa Biden.

Buttigieg amesimamia mizozo kadhaa ya umma akiwa Waziri wa Uchukuzi.

Alisaidia kusimamia juhudi za serikali baada ya ajali ya treni katika kijiji cha East Palestina katika jimbo la Ohio, kuporomoka kwa Daraja la Baltimore na mzozo wa ratiba wa Shirika la Ndege la Southwest 2022.

Gavana wa Pennsylvania, Josh Shapiro

sd

Chanzo cha picha, Getty Images

Gavana huyo, ambaye hapo awali aliwahi kuwa mwanasheria mkuu wa serikali, amefanya kazi katika nyadhifa mbalimbali za chama wakati wa uongozi wake.

Aligonga vichwa vya habari mwaka jana baada ya kujenga upya daraja lililoporomoka kwenye barabara kuu ya Philadelphia - ushindi mkubwa wa kisiasa kwa gavana wa awamu ya kwanza.

Ukarabati huo wa haraka ulisifiwa na wengi kama njia bora ya mazungumzo ya kisiasa katika miundombinu kwa mgombeaji wa urais 2028.

Gavana wa Illinois, JB Pritzker

d

Chanzo cha picha, Getty Images

JB Pritzker, gavana wa Illinois, ameinua hadhi yake katika miaka ya hivi karibuni kwa kumshambulia Trump na kumtetea Biden.

Mfanyabiashara bilionea - mrithi wa hoteli za Hyatt - ni mwepesi wa kuchapisha ukosoaji kwa Trump kwenye mitandao ya kijamii.

Baada ya mdahalo alimuita Trump "mwongo" na kusema yeye ni "mtuhumiwa wa makosa 34 ambaye anajijali yeye pekee."

Kama Whitmer, Pritzker ana rekodi ya kuweka kanuni za kulinda masuala ya haki za uavyaji mimba na udhibiti wa bunduki.

Wagombea wengine ni nani?

m

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Michelle Obama

Gavana wa Kentucky, Andy Beshear, gavana wa mihula miwili katika jimbo la kihafidhina, amepata uungwaji mkono kitaifa tangu kuchaguliwa tena mwaka jana.

Gavana wa Maryland, Wes Moore amejikuta kwenye macho ya wengi katika miezi ya hivi karibuni kufuatia kuporomoka kwa Daraja kubwa la Francis Scott huko Baltimore.

Maseneta Amy Klobuchar na Cory Booker hutajwa mara kwa mara, kwani waliwahi kuwania urais siku za nyuma na wana kubalika miongoni mwa wana-Democratic.

Seneta wa Georgia Raphael Warnock, alishinda kinyang'anyiro cha useneta uliokuwa na ushindani mkubwa, pia ametajwa kuchukua nafasi ya Biden.

Kura ya maoni ya Reuters IPSOS iliyotolewa Jumanne inaeleza kuwa mtu pekee anaeweza kumshinda Trump Novemba ni Michelle Obama. Ingawa mke wa rais wa zamani amesema mara kwa mara hana matarajio ya kugombea urais.

Pia unaweza kusoma

Imetafsiriwa na Rashid Abdallah na kuhaririwa na Yusuf Jumah